LOGO

KLABU zote za Ligi Kuu zikiwamo Simba na Yanga zimetoa siku saba kwa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi kufanyia kazi mapendekezo yao ya kutokatwa asilimia tano za mgawo wao wa wadhamini wa ligi hiyo vinginevyo watagomea ligi hiyo. Klabu za Ligi Kuu Bara zinapokea fedha za udhamini Sh73 milioni kutoka Vodacom na Sh110 milioni kutoka Azam TV ambazo asilimia tano yake ni Sh9.15 milioni na kwa klabu 14 za ligi hiyo  TFF itapata Sh128 milioni. Klabu hizo kupitia mwanasheria wao, Damas Ndumbaro, amesema kuwa endapo mapendekezo yao yatashindwa kufanyiwa kazi kwa siku walizotoa basi watachukua hatua mbalimbali ili kupata haki yao ikiwamo kufungua kesi ya malalamiko katika Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa). Pia Ndumbaro alisema wataungana kugomea ligi hiyo hadi watakapopata haki yao, lakini watahakikisha wanamfikisha mahakamani yeyote atakayebainika kukata makato hayo kinyume na utaratibu. “Rais amesisitiza makato haya ya asilimia tano kinyume na taratibu kwani waliopitisha mchakato huu siyo klabu zenyewe, watu wa bodi waliokuwapo katika kikao hawakukubali makato haya ndiyo maana hadi leo TFF hawajatoa taarifa za kikao hicho,” alisema Ndumbaro.
Juzi Alhamisi Malinzi alitoa tamko kwamba ni lazima klabu zikatwe asilimia tano kutoka kwa wadhamini wao ambazo ni kwa ajili ya mfuko wa maendeleo ya soka la vijana na Ligi ya Wanawake. Ndumbaro alisema wanaikaribisha TFF mezani ili kujadili mchakato huo lakini msimamo mwingine kama Malinzi hatabadili msimamo ni kugomea kuvaa jezi za Vodacom ambao ni wadhamini wao.  Mwanasheria huyo alienda mbali kwa kusema wametoa ombi la kukaguliwa kwa matumizi ya fedha  TFF tangu uongozi wa Malinzi ulipoingia madarakani Oktoba 2013. Ndumbaro alisema kuwa wateja wake ambao ni klabu 14 za Ligi Kuu Bara wanalalamikia kukatwa asilimia tano kutoka Vodacom na Azam TV kinyume na makubaliano ya mkataba wao na haraka wanataka kukaa meza moja na Malinzi ili kumaliza tatizo hilo. “Tumeonyesha nia ya kutokuwa na imani na Malinzi pamoja na uongozi wake kwa jinsi wanavyosisitiza mchakato huu. Tutaomba mkutano mkuu wa dharura ambapo wanachama ndiyo walioichagua Bodi ya Ligi na wana uwezo kuifanya bodi iwepo ama isiwepo ili kupiga kura za kusudio la kutomwamini Malinzi,” alisema Ndumbaro. Ndumbaro alisema TFF wana mgao wao wanaupata kutoka Vodacom na Azam TV kwa ajili ya mambo ya uendeshaji hajui ni kwa nini wanaendelea kuzinyonya klabu.

0 comments Blogger 0 Facebook

Chapisha Maoni

ZILIZOSOMWA SANA

 
TASWIRA MICHEZONI © 2015. All Rights Reserved. This Blog Proudly Designed by MMC™ Media Group Ltd | Phone +255-786-758-021
Top